Thursday, July 29, 2010

Azam FC JKT Ruvu Ruvu sare ya 1-1, kucheza na Simba usiku kesho Amaan Stadium





Zikicheza soka la kuvutia wakati wote wa mchezo, timu za Azam FC na JKT Ruvu zimetoshana nguvu kwa kufungana goli 1-1 katika mchezo wa kuvutia wa kirafiki uliochezwa kwenye dimba lililokarabatiwa wa Amaan visiwani Zanzibar.

Azam FC ndiyo waliokuwa wa kwanza kupata goli katika dakika ya 25 lililofungwa na Ibrahim Mwaipopo kwa njia ya penati baada ya beki wa JKT Ruvu Stephano Nkomola kuunawa mpira katika eneo la hatari

Bao la JKT Ruvu lilifungwa katika dakika ya 85 baada ya mchezaji mpya wa JKT Ruvu Pius Kisambale kuukwamisha wavuni mpira wa krosi toka wingi wa kulia.

Katika mchezo wa leo, mchezaji Kalimangonga Ongala ambaye aliingia kipindi cha pili alikonga nyoyo za mashabiki kutokana na kuonesha soka la hali ya juu. Kaly alikuwa fundi sana wa kuuficha mpira, alikuwa na nguvu sana za kupambana lakini zaidi ya yote alikuwa na spidi ya kutosha na ameonesha matumaini makubwa sana.

Mchezaji Mrisho Ngasa kama kawaida yake aling’ara sana uwanjani akicheza kwa kiwango chake cha siku zote. Licha ya kupoteza nafasi mbili tatu za kufunga Ngasa alikuwa hatari muda wote wa mchezo.

Ibrahim Mwaipopo ambaye ameonekana kuongezeka misuli na spidi leo amecheza soka la hali ya juu sana, mwaipopo ana sifa iliyojificha nayo ni uwezo wa kuutuma mpira umbali mrefu na mpira ukafika pahala alipokusudia, leo ndicho kitu alichukuwa akikifanya Ibrahim, alikuwa akipiga pasi ndefu kulia na kushoto na zilikuwa zikifika barabara, penati yake aliifunga kwa ufundi mkubwa sana ambapo mpira ulianza kugonga mwamba wa juu kabla ya kutinga nyavuni. inaonekana kama licha ya kuja nyota kibao wa sehemu ya kiungo lakini nyota huyo wa Tanzania anaelekea kuilinda nafasi yake vizuri.

Tuseme nini kuhusu Jabir Aziz? Kama kuna mchezaji ambaye Azam FC imelamba dume kwenye usajili basi ni chipukizi huyu. Kwa wanaofuatilia soka la kimataifa na wanaomjua vizuri Xavi Harnandes wa FC Barcelona basi kwa huku bongo jabir ni photocopy na Xavi, Jabir leo alikuwa kila sehemu uwanjani akimiliki mipira na kuisambaza kwa wahusika utadhani mashine. Ama hakika atakaporudi Salum Abubakar toka timu ya Taifa ya Vijana Azam FC itatisha sehemu ya katikati.

Leo kwa mara ya kwanza kwenye kikosi cha Azam FC tumeshuhudia mapacha wawili sehemu ya ulinzi, Ibrahim shikanda upande wa kulia na Patrick Mafisango upande wa kushoto. Nawaita mapacha kutokana na aina ya uchezaji wau kwa lugha ya kiingereza ningeweza kuwaita stylish players. Kama ilivyo Shikanda, Mafisango alikuwa akicheza kwa nidhamu na ufundi mkubwa sana, anakaba kwa kutumia akili sana, anaelekeza wenzake nini cha kufanya, ana mbinu na ujuzi wa kuwasoma wapinzani kwa haraka lakini zaidi ya yote ana kipaji cha kumiliki mpira na hawa ni wachezaji ambao hawakupoteza pasi leo uwanjani.



John Bocco Adebayor leo alikuwa burudani…. Alikuwa akimiliki mipira vizuri na kuigawa kwa wenzake lakini pia wakati alipotakiwa kupiga alipiga na kulenga goli vizuri. Bocco ambeye ndiye mfungaji bora wa Azam FC wa wakati wote akiwa na miaka 20 tuu ameonesha kuwa mazuri mengi bado hayajaiva na yanaendelea kuja toka kwa kijana huyu mrefu mwenye uwezo wa kupiga kwa miguu yote na kichwa.

Aggrey Morris na Eraso Nyoni wameonesha kuwa wao ndiyo pacha bora ya Azam FC kwa upande wa walinzi wa katikati. Aggrey ana Nguvu nyingi sana na Erasto ana akili nyingi sana. Mchanganyiko huu ni mzuri sana kwenye timu na ndicho walichokionesha uwanjani, walikuwa wakipeana majukumu vizuri sana na inaonekana kwamba msimu huu tutakuwa na kikosi bora kabisa.

Mechi nyingine ni keshokutwa ambapo Azam FC itacheza usiku na Simba SC

Wednesday, July 21, 2010

Azam fc yaibanjua Ruvu Shooting






Baada ya kutoa sare na Ngorongoro Heroes, Azam FC leo imepata ushindi wa 2-1 dhidi ya timu ya Ruvu Shooting katika uwanja wa Ruvu Mkoani Pwani.

Azam FC ilianza kupata goli la kwanza dakika ya 15 ya mchezo lililofungwa na mchezaji John Bocco baada ya kuunganisha krosi ya Faraji Hussein.

Goli hilo lilidumu kwa dakika 20, baada ya beki wa kutumainiwa wa Azam FC, Aggrey Morice kuandika goli la pili kwa mpira wa kichwa baada ya kuunganisha mpira wa adhabu ndogo uliyopigwa kiufundi na Ibrahim Mwaipopo.

JKT walipata penati katika dakika za mwisho kipindi cha kwanza lakini golikipa mpya wa Azam Jackson Chove aliokoa

Matokeo hayo yalizipeleka timu zote mbili mapumziko, huku Azam FC ikiongoza kwa 2-0.

Kipindi cha pili tiu Azam FC ilifanya mabadiliko kuimarisha ngome yake kwa kumtoa Erasto Nyoni na Seleman Kassim ‘Selembe’ na nafasi zao zikachukuliwa na Salum Swed na Jamal Mnyate.

Dakika ya 51 Ruvu Shooting walipata goli kupitia kwa mchezaji Salum Kimai baada ya kuachia shuti lililotinga wavuni na kumuacha kipa wa Azam FC, Jackson Chove akishangaa.

Goli hilo lilileta mabadiliko ya mchezo kwani timu zote zilicheza kwa kukamiana huku Ruvu Shooting wakitaka ushindi katika mechi yao ya nyumbani, na Azam wakiitaji kulinda lango wasipoteze mechi ya leo.

Katika mechi hiyo ya kirafiki, golikipa Jackson Chove alipewa kadi nyekundu baada ya kumkanyaga mchezaji Paul Ndauka na mchezaji wa Ruvu Shooting Gido Chawala alipewa kadi nyekundu baada ya kumsukuma Chove baada ya kumfanyia madhambi Ndauka.

Kocha wa Azam FC,Itamar Amorin amesema kikosi chake kimebadilikana kuimarika kuliko walipokuwa wakicheza mechi yao ya kwanza.

“Timu imecheza vizuri, kuna mabadiliko makubwa hasa upande wa pasi, ball position na ball control ukilinganisha na mechi iliyopita, kwani wameimarika zaidi.” Alisema Itamar.

Ameongeza amerekebisha makosa yaliyotokea katika mechi dhidi ya Ngorongoro, na kuifanya timu hiyo kuwa katika hali nzuri zaidi.

Akizungumzia uwanja wa Ruvu, Itamar alisema ni uwanja mzuri, una nyasi nzuri lakini zimezidi sana na hazifai kwa kuchezea mpira kwani mpira unakwama mara na kupoteza pasi za wachezaji.

Azam FC, Jackson Chove/David Mwasongwe, Ibrahim Shikanda/Malika Ndeule, Mau Bofu, Agrey Morice, Erasto Nyoni/Jamal Mnyate, Ibrahim Mwaipopo, Faraji Hussein/Ally Mkuba, Ramadhani Chombo ‘Ridondo’, John Bocco/Ally Manzi, Mrisho Ngassa/Cosmas Lewis, Seleman Kassim/ Jamal Mnyate.

Yonatus Mbalimo, Mangasin Mbomus, Peter Moses, George Akitenda, George Osey, Owen Mikumba, Godo Chawala, Faraji Makumbo, Martin Lupati, Salum Chimai, Revocatus Maliwa.

Thursday, July 15, 2010

Mambo ya Chamazi












Picha hizi zinaonesha maendeleo ya ujenzi wa kituo cha michezo cha Azam FC ambapo kwa mujibu wa Ramani ya Ujenzi kutakuwa na Bwawa la kuogelea la kiwango cha Olympic, hostels za wachezaji, kiwanja cha mazoezi cha nyasi bandia kama kile cha Karume, kiwanja cha mazoezi kingine cha nyasi za kawaida kama za uwanja mpya wa Taifa na uwanja mkubwa wa michezo.

Ujenzi wa kituo hiki unafanywa kwa Awamu ambapo awamu ya kwanza inahusisha hostels za wachezaji, kiwanja cha mazoezi cha nyasi bandia, bwawa la kuogelea, kanteen ya chakula na Uzio wa eneo lote.



Azam Kuwa na Uwanja wake

Habari kwa hisani ya gazeti na Mwananchi

KLABU ya Azam imetangaza kikosi chake na kuweka bayana ujenzi wa uwanja wao kisasa huko Chamanzi Jijini Dar es Salaam na kuhaidi kuanza kutumia kwenye michezo yake ya Ligi Kuu katika mzunguko wa pili.

Klabu hiyo itakuwa ya kwanza hapa nchini kujenga uwanja wa kisasa ambao utakuwa ukitumika kwenye michezo ya Ligi Kuu.

Mwenyekiti wa Azam, Said Mohamed alisema kuwa tayari wameshaingia mkataba na kampuni moja iliyopo Afrika Kusini kwa ajili ya kujenga uwanja huo kwa kutumia nyasi za bandia.

Alisema mbali na nyasi hizo wameshaanza ujenzi wa hosteli za wachezaji wao ambazo zitatumika kama kambi ya wachezaji na zitaanza kutumika rasmi mzunguko wa pili ya Ligi Kuu Tanzania bara unaoanza Agosti 21.

Pia, kambi hiyo itakuwa na kila kitu ambacho ikiwemo sehemu ya kufanyia mazoezi ya viungo ( GYM) ambayo itatumika kwa wachezaji wao kufanya mazoezi ya viungo.

Kwa upande wa wachezaji wanaowaacha mwenyekiti huyo alisema kuwa timu yao imesajili 22 na vijana chini ya miaka 20 sita.

Wachezaji walioacha ni Chrispine Wadenya, Hadid Mhana, Maridad Haule, Nsa job, Said Swed, Salum Machaku, Yahaya Tumba, Ben Kalama, Shaban Kisiga na Dan Wagaluka.

Waliowasajili wapya kwa ajili ya msimu ujao ni Mohamed Binslum, Jackson Chove, Jabil Azizi, Mrisho Ngassa, Kali Ongala ( GIF Sweden) Mutesa Patrick (APR Rwanda) na Ssenyonjo Peter (Polisi Uganda).

Kocha wa timu hiyo Amorian Itamaa alisema kuwa kuacha kwa wachezaji hao wameangalia vitu vingi ikiwemo nidhamu na kushuka kwa uwezo wake uwanjani.

Alisema kunabaadhi ya wachezaji wamekuwa na nidhamu mbaya katuika kambi na mazoezini na wengine wameshuka uwezo ndio maana tumewaacha katika usajili wetu mpya.

Aidha alisema kuwa mchezaji yoyote yule hawe na jina hasiwe na jina kama hatakuwa na midhamu mbaya atawajibishwa kwani msimu huu wamejipanga kuchukua ubingwa wa ligi kuu.

Hata hivyo wachezaji wote waliosajiliwa na klabu hiyo wameingia kambini katika ufukwe wa Bamba beach uliopo Kigamboni nje kidogo ya Dar es Salaam.


Ngasa Hajaacha pengo, asema papic


Habari kwa hisani ya Habari leo

KOCHA Mkuu wa Yanga Kostadin Papic amesema aliyekuwa mshambuliaji wa timu hiyo Mrisho Ngasa hajaacha pengo katika timu hiyo, ila ameacha nafasi, ambayo imeshazibwa.


Papic akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya mazoezi ya timu hiyo katika Uwanja wa Uhuru Dar es Salaam jana, alisema.

Ngasa ameacha nafasi ambayo imeshazibwa na wachezaji wengine na sio pengo kama wengi wanavyodhania.

Papic alisema kimsingi nafasi ya mchezaji huyo imejazwa na wachezaji Shamte Ally, Nsa Job na Kenneth Asamoah ambao anaamini wanaweza kuisaidia Yanga kama alivyofanya Ngasa.

Mshambuliaji Kenneth Asamoah alisaini kuichezea Yanga akitokea nchini Ghana wakati Nsa Job amejiunga na klabu hiyo baada ya kutupiwa virago na timu yake ya zamani ya Azam FC.

Ally alikuwepo Yanga wakati wa Ngasa. Papic alisema kwamba kimsingi timu haiwezi kuundwa kwa kumtegemea mchezaji mmoja bali mchezaji mmoja anaweza kuwa sehemu ya timu.

Ngasa winga hatari wa klabu hiyo alisaini mkataba wa miaka mitatu kuichezea Azam, uhamisho uliogharimu Sh milioni 58.

Anayemtaka Boban atapaswa kulipa 80Milioni


Habari kwa hisani ya Habari leo
KAMPUNI ya wakala wa wachezaji ya Ndumbaro Soccer Agency ambayo ilifanikisha mchezaji Haruna Moshi ‘Boban’ kwenda kucheza soka la kulipwa nchini Sweden imesema kiungo mshambuliaji huyo amepotoka kuamua kuvunja mkataba wake na klabu ya Gefle IF na kurejea nchini.

Wakala wa mchezaji huyo anayetambulika na Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), Damas Ndumbaro amesema kutokana na kupotoka huko kiungo huyo amekosa nafasi ya kuweka rekodi ya kuwa mchezaji wa kwanza wa Tanzania kucheza michuano ya Ligi ya Ulaya, ambayo klabu hiyo imefuzu kucheza.

Ndumbaro alibainisha hayo jana wakati akitoa ufafanuzi kuhusiana na kurejea nchini kwa Boban baada ya mchezaji huyo kuripotiwa na vyombo vya habari akidai aliamua kuachana na timu hiyo ya Sweden kutokana na maslahi madogo, ubabaishaji na kudhulumiwa fedha.

Boban alivunja mkataba na klabu hiyo Julai 4 mwaka huu na kurejea nyumbani akidai anataka kuichezea klabua yake ya zamani ya Simba, ingawa jana aliripotiwa akisema bado hadi sasa hajapata timu ya kuichezea.

Kwa mujibu wa Ndumbaro, Boban alikuwa anapata malipo yake yote ambayo ni krona 40,000 ambazo ni sawa na dola za Marekani 5,000 kwa mwezi na alipatiwa nyumba yenye samani ndani alichotakiwa ni kulipa kodi ya mwezi.

Pia alisema alikuwa akipata maslahi mengine kama kulipwa posho ya dola 200 kila anapocheza mechi, lakini asipocheza mechi kwa sababu binafsi hukatwa sehemu ya mshahara wake.

“Mbali na hayo alikuwa apewe tiketi mbili za ndege za kusafiria kwenda na kurudi wakati wa likizo na zaidi ya hayo fedha za mshahara ambazo alikuwa anakatwa kodi kwa mujibu wa sheria za Sweden angerudishiwa pindi mkataba wake unapomalizika na kutokana na yeye kuvunja mkataba huo fedha hizo sasa zinafanyiwa utaratibu ili aweze kupewa,” alisema Ndumbaro.

Ndumbaro alibainisha kuwa Aprili mwaka huu alipokea taarifa kuwa Boban ameomba kuvunja mkataba, baada ya kutokubaliana na Klabu ya Gefle IF kuhusiana na matakwa yake ya kutaka mshahara wake usikatwe kodi.

Boban aliyesaini mkataba wa miaka miwili wa kuichezea Gefle IF kwa uhamisho wa dola za Marekani 55,000 aliyerejea nchini hivi karibuni akitokea Sweden na kudai hivi sasa ni mchezaji huru, jambo ambalo wakala wake ameamua kulitolea ufafanuzi na kubainisha kuwa hayuko huru na klabu ambayo itataka kumsajili itahitajika kumlipa wakala.

“ Kutokana na mkataba uliopo klabu ya Gefle IF inatakiwa ilipwe dola 55,000 ambazo ni sawa Sh milioni 82 za Kitanzania na Ndumbaro Soccer Agency wanatakiwa walipwe asilimia 10 ya kiasi hicho cha fedha ambacho Gefle walitoa kama ada ya uhamisho wa Boban,” alisema Ndumbaro.

Aidha Ndumbaro alisema wao wanapenda kumwona Boban akiendelea kucheza soka na klabu ambazo zinamhitaji zinatakiwa kutambua makubaliano ambayo yalitiwa saini na mchezaji huyo wakati akienda kucheza Gefle IF.

Lakini alipoulizwa jana kuhusiana na suala hilo, Boban alisema yeye hafuati heshima badala yake anafuata fedha na ndicho anachojali. “Kuwa wa kwanza maana yake nini, mimi naangalia maslahi ninayoyapata, siangalii mambo mengine. “Nahitaji fedha, hayo masuala ya heshima hayanihusu,” alisema Boban.

Hata hivyo alipoulizwa kuhusiana na madai mengine ikiwemo kutaka apewe fedha zinazotokana na viingilio, mchezaji huyo alisema hakuwa tayari kuzungumzia jambo hilo.

“Kwa sasa siwezi kuzungumzia, kama wakala anazungumza muache azungumze, kwani mtu hakatazwi kusema,” alisema Boban na kuomba atafutwe baadaye kwa ufafanuzi zaidi, ambapo alipotafutwa baadaye simu yake ilikuwa imezimwa.

Naye Clecence Kunambi anaripoti kuwa, wachezaji Thomas Ulimwengu na Yusuf Saidi walioenda nchini Sweden kufanya majaribio ya kucheza soka la kulipwa katika Klabu ya daraja la kwanza ya Dalkurd FF wamefuzu majaribio yao.

Kabla ya kwenda Sweden Ulimwengu alikuwa mchezaji wa kituo cha michezo cha Tanzania Soccer Academy, ambapo pia aliongezwa kwenye kikosi cha timu ya Moro United, wakati Yusuf Said alionekana katika mashindano ya Copa Coca-Cola akiwa na timu ya Kigoma.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini jana, Ndumbaro alisema wachezaji hao wote walifanikiwa kupita katika majaribio yao na sasa wapo katika mazungumzo ya kusaini mkataba na klabu hiyo.

Alisema anajivunia rekodi ya wachezaji anaowapeleka nje kucheza soka kufuzu katika majaribio yao. Aliwataja wachezaji hao kuwa ni Boban, Joseph Kaniki ambaye baadaye alishindwa kuchezea timu hiyo kutokana na kuwa na mkataba na klabu ya Rayon ya Rwanda na Jerry Tegete ambaye hata hivyo Yanga ilimzuia kwenda.

Tuesday, July 13, 2010

Azam yatangaza usajili 2010, yamtwaa rasmi Patrick mafisango, Ngasa haendi kokote




ikiwa imesalia siku moja kufikia mwisho wa usajili kwa ajili ya msimu ujao wa ligi kuu utakaoanza August mwaka huu, uongozi wa Azam FC umetangaza kukamisha usajili wake na kuanza kwa maandalizi kwa ajili ya ligi hiyo.

Makamu Mwenyekiti wa Azam FC, Said Mohamed amesema usajili wa mwaka huu wameacha wachezaji kumi waliokuwepo msimu ulipita na kubakisha wachezaji 14, huku wakisajili wachezaji wapya nane na kupandisha jumla ya wachezaji sita kutoka katika timu ya vijana 'Azam Academy'.

“Katika usajili wetu tumesajili wachezaji watatu kutoka nje ya Tanzania na watano kutoka katika vilabu vya hapa nchini, tumezingatia taratibu za TFF kwa kusajili wachezaji wa kigeni wasiozidi watano, ni matumaini yetu wachezaji wetu watafanya vizuri” alisema Mohamed.

Mohamed aliongeza kuwa Azam itakuwa na jumla ya wachezaji watano wa kigeni baada ya kuongeza wachezaji watatu ambao wataungana na wengine wawili walipo katika timu hiyo.

Uongozi umewataja wachezaji wapya waliosajiliwa na timu hiyo kuwa ni Mohamed Binslum (Huru) Jackson Chove(JKT Ruvu), Jabir Aziz na Ramadhan Chombo 'Redondo' (Simba), Mrisho Ngassa (Yanga), Kalimangonga Sam Daniel Ongala Rampling 'Kali Ongala' (GIF-Sweeden), Patrick Mutesa Mafisango (APR- Rwanda) na Peter Senyonjo (Polisi-Uganda.)

Wachezaji waliobaki ni John Bocco, Erasto Nyoni, Jamal Mnyate, Salum Aboubakar 'Sure Boy', Vladmir Niyonkuru, Philip Alando, Luckson Kakolaki, Malika Ndeule, Aggrey Morice, Salum Swed, Ibrahim Shikanda, Ally Manzi, Seleman Kasim 'Selembe' na Ibrahim Mwaipopo.

Makamu Mwenyekiti aliongeza kuwa timu hiyo haikuwaacha mbali wachezaji wao wa timu ya vijana 'Azam Academy', imepandisha wachezaji sita ambao ni Sino Augustino, Himid Mao, Mau Ali, Tumba Swed, Ali Mkuba na Samih Nuhu.

Mohamed aliwataja wachezaji walioachwa kuwa ni Chrispin Odula, Habib Mhina, Maridad Haule, Nsa Job, Said Swed, Salum Machaku, Yahya Tumbo, Ben Kalama, Shaaban Kisiga na Dan Wagaluka.

Azam kambini Bamba beach Kigamboni.

Timu ya Azam FC kesho inataraji kuweka kambi Bambabay maeneo ya Kigamboni jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kufanya maandalizi ya ligi kuu.

Azam FC ikiwa kambini itakuwa ikifanya mazoezi mara mbili kwa siku, asubuhi itakuwa ikitumia uwanja wa Uhuru na jioni kufanya mazoezi katika viwanja vilivyopo Kigamboni.

“Tumeamua kwenda Kigamboni kutokana na kupata eneo zuri kwa ajili ya kambi, pia kuna viwanja vizuri vya kufanyia mazoezi” alisema mwenyekiti wa Azam FC, Said Mohamed.

Aliongeza kuwa timu itakuwa huko kwa muda maalum huku ikisubiri taarifa maalum kutoka TFF kama kutakuwa na safari ya kwenda ufaransa, kama haitakuwepo timu itaenda Zanzibar kwa ajili ya maandalizi

Wachezaji wapya

Mohamed Binslum (Huru)

Jackson Chove(JKT Ruvu)

Jabir Aziz na Ramadhan Chombo 'Redondo' (Simba)

Mrisho Ngassa (Yanga)

Kalimangonga Sam Daniel Ongala Rampling 'Kali Ongala' (GIF-Sweeden),

Mutesa Mafisango (APR- Rwanda

Peter Senyonjo (Polisi-Uganda.)

Wachezaji waliobaki

John Bocco,

Erasto Nyoni

Jamal Mnyate

Salum Aboubakar 'Sure Boy'

Vladmir Niyonkuru

Philip Alando

Luckson Kakolaki

Malika Ndeule

Aggrey Morice

Salum Swed

Ibrahim Shikanda

Ally Manzi

Seleman Kasim 'Selembe'

Ibrahim Mwaipopo

Waliopandishwa Kutoka Azam Academy

Sino Augustino

Himid Mao

Mau Ali

Tumba Swed

Ali Mkuba

Samih Nuhu

walioachwa

Chrispin Odula

Habib Mhina

Maridad Haule

Nsa Job

Said Swed

Salum Machaku

Yahya Tumbo

Ben Kalama

Shaaban Kisiga

wageni wafunika mazoezini

Kutoka mazoezini leo, tovuti imegundua kuwa wachezaji wapya waliojiunga na timu ya Azam FC wanafanya vizuri hali iliyompa matumaini kocha Itamar Amorin.

Azam FC imefanya usajili kwa kuongeza wachezaji wapya ili kuimarisha kikosi hicho ambacho kina malengo ya kuwa nafasi ya juu katika ligi kuu ijayo.

Wachezaji wapya walikuwepo mazoezini leo ni Mrisho Ngassa, Ramadhani Chombo 'Ridondo', Jackson Chove, Mohamed Slum, Kally Ongala na Jabir Aziz.

Wachezaji hao wameonekana wakishirikiana vyema na wachezaji waliokuwepo katika timu hiyo, ushirikiano huo kama utaendelea vizuri, timu itakuwa katika nzuri zaidi.Kutoka mazoezini leo, tovuti imegundua kuwa wachezaji wapya waliojiunga na timu ya Azam FC wanafanya vizuri hali iliyompa matumaini kocha Itamar Amorin.


Kama safari ya Ufaransa ipo, basi ni matunda ya jitihada zetu


Ikiwa ni mara ya kwanza kwa timu tatu bora za ligi kuu ya Tanzania kupata mualiko wa kufanya mazoezi nchini Ufaransa, Timu ya Azam FC imepata nafasi hiyo na kuichukulia kama sehemu yao ya mafanikio.

Kocha Itamar Amorin amesema jitihada walizofanya msimu uliopita ndizo zilizopelekea timu kuwa nafasi ya tatu na kupata mualiko huo wa kwenda Ufaransa.

“Tulikuwa na malengo ya kuwa katika nafasi ya nne lakini tulipoongeza bidii katika mazoezi na mechi zetu tukafanikiwa kuwa katika nafasi ya tatu ambayo imetuwezesha kupata nafasi ya kuwa mmoja ya waalikwa wa kwenda Ufaransa, kama tusingekuwa hgrkatika nafasi ya tatu tusingepata mualiko huo.” alisema Itamar.

Aliongeza kuwa kama timu itapata uthibitisho rasmi wa kwenda Ufaransa, itatumia safari hiyo kama sehemu ya majaribio kama ilivyo katika program ya mazoezi ya kujiandaa na ligi kuu ijayo.

Itamar alisema kuwa mipango ya kufanya mechi za majaribio ikiwa ni sehemu ya maandalizi itategemea na safari ya kwenda Ufaransa kama safari haitaingiliana na siku za mechi za majaribio, kutakuwa na mechi hizo.

Msimu mpya jezi mpya


Msimu mpya na mambo mapya, Azam FC wameanza mazoezi wakiwa na jezi mpya tofauti na zile walizokuwa wakizitumia msimu ulipoita.

Azam ya sasa ikiwa mazoezini inavaa jezi zenye rangi ya bluu iloyoiva yenye rangi ya chungwa mabegani, huku wakitumia kaptura nyeusi zilizo na mchirizi wa rangi ya chungwa, namba za wachezaji na maandishi ya Azam yanarangi ya chungwa.

Makocha msimu huu wanavaa jezi nyeupe zenye mistari miwili ya rangi za blu pembeni, huku kaptura zao zikiwa nyeupe na mistari miwili ya rangi za blu, jezi hizo zina maandishi yenye rangi za chungwa.

Msimu uliopita Azam FC walikuwa wakitumia jezi zilizokuwa katika mfumo wa Tshirt zenye rangi ya chungwa, na makocha walikuwa wakivaa jezi za rangi nyeupe na bluu bahari.

Azam kucheza na Ngorongoro jumamosi


Timu ya Azam siku ya Jumamosi itakuwa ikifanya mechi yake ya mazoezi dhidi ya timu ya taifa ya vijana chini ya miaka ishirini U20, Ngorongoro Heroes, katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

Ikiwa ni mechi ya kwanza ya majaribio kwa timu ya Azam FC, itatumia fursa hiyo kuwapa mazoezi Ngorongoro Heroes ambao wapo katika maandalizi ya kucheza mechi yakufuzu kucheza fainali za Afrika kwa vijana dhidi ya Ivory Coast mwishoni mwa mwezi huu.

Kocha Itamar amesema, mechi hiyo itakuwa muhimu pia kwa timu ya Azam ambayo itakuwa ikifanya maandalizi kwa ajili ya safari ya Ufaransa na ligi kuu ijayo.

“Ngorongoro ni timu imara na nzuri, italeta ushindani mkubwa kwa Azam kwani ina majaribio yake ya kwanza kwa yatakayosaidia kujua uwezo wa timu mapema ili kurekebisha sehemu zitakazokuwa na mapungufu.” aliongeza Itamar.

Sunday, July 11, 2010

Wenger amsalandia Ngasa


NYOTA njema imeanza kumuelekea mchezaji mahiri nchini Mrisho Ngasa, baada ya Kocha Mkuu wa Arsenal ya England, Arsene Wenger kueleza kuwa amekunwa na kipaji chake.

Wenger alimuona Ngasa Jumatatu kupitia televisheni katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa kati ya timu ya Taifa ya Brazil na timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ uliofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kulingana na taarifa ya mtandao wa KickOff.com wa Afrika Kusini, kiwango cha Ngasa ambaye msimu uliopita wa Ligi Kuu Tanzania Bara alichezea Yanga na sasa amesaini Azam ambayo pia inashiriki ligi hiyo ni cha juu na atatafuta taarifa zake zaidi.

“Afrika ni mgodi wa dhahabu katika soka na kipaji kinasubiri kuibuliwa, usiku uliopita (Jumatatu), nilitazama mchezo baina ya Brazil na Tanzania.

“Tanzania walifungwa mabao mengi, lakini kulikuwa na wachezaji wawili ambao niliwaona, mmoja ni mfano wa aina ya uchezaji wa Walcott (Theo), ambaye alinifanya niseme mara moja kuwa, ninahitaji kujua zaidi, habari zake ,” alikaririwa Wenger.

Hata hivyo kocha huyo hakumtaja kwa jina Ngasa ambaye mwaka jana alienda kufanya majaribio timu ya West Ham inayoshiriki Ligi Kuu England na kukwama, lakini Ngasa ndiye anayecheza kama Walcott.

Kocha huyo mwenye sera ya wachezaji vijana, aliweka wazi kuwa yeye ni shabiki mkubwa wa timu ya Taifa ya Brazil.

“Inawezekana ikatokea Brazil wakashinda michuano hii, lakini hawana vipaji vya ubunifu kama vile ambavyo walikuwa navyo kikosi chao kilichopita na hilo ndilo linanifanya nifikirie kuwa watakuwa na wakati mgumu katika michuano hii,” alisema.

Wenger anaamini kikosi cha timu ya Ivory Coast ‘The Elephants’ ndicho pekee cha Afrika ambacho kinaweza kupambana na kuleta ushindani katika kuwania Kombe la Dunia katika michuano inayoanza kutimua vumbi leo nchini Afrika Kusini.

Akizungumza kwenye hafla ya Castrol Index iliyofanyika Sandton, Afrika Kusini na kunukuliwa na mtandao huo, kocha huyo Mfaransa alisema anaamini kuwa Ivory Coast ina kikosi imara ambacho kinaweza kutoa upinzani kwa miamba wengine wa soka bila ama ikiwa na nyota wake Didier Drogba.

“Endapo Didier Drogba hatokuwa fiti, bado Ivory Coast ina wachezaji bora na kwenye suala la ushambuliaji hawajapungukiwa,” Wenger aliuambia mtandao huo.

“Endapo unataka kutazama kuhusiana na viwango vya timu, unatakiwa kutazama ni wachezaji wangapi wanacheza kwenye klabu kubwa na pengine kuna klabu kubwa kumi duniani na wana asilimia kubwa ya wachezaji katika klabu kubwa hizo kwa hiyo wana uwezo mkubwa, ingawa wako kwenye kundi gumu.

“Timu ya pili ambayo naiona inaweza kuleta ushindani ni Cameroon, wana wachezaji wazuri lakini inaonekana hawajajiandaa vyema katika maandalizi yao kwa ajili ya michuano hii.

“Kwa ujumla sina hakika kama hawana matatizo ya ndani, ambayo yanawatatiza hali inayosababisha hali hiyo,” alisema.
Wenger pia anaamini Bafana Bafana inaweza kucheza katika raundi za mwisho za michuano hiyo.

“ Swali ni kwamba Afrika Kusini ina timu nzuri ambayo imefanya katika mechi zake za maandalizi, lakini inaonekana kidogo inakosa viwango.”

Alipoulizwa ni mchezaji yupi anaamini ataibuka kuwa nyota mpya wa Afrika, Wenger alijibu kuwa: “Sijui jibu la swali hilo na kwa sasa hakuna mtu huyo, lakini katika michuano hii ya Kombe la Dunia itakuwa ni nafasi nzuri na kubwa ya kuona nani atakuwa nyota mpya wa Afrika."

Alipoulizwa kuhusiana na timu zipi anadhani zitafuzu kucheza kwenye hatua ya nusu fainali ya Kombe la Dunia, alizitaja timu hizo kuwa ni Hispania , Argentina, England na Uholanzi.


Sunday, June 27, 2010

kumbe Nadir Haroub Canavaro yupo huru

WACHEZAJI Mussa Hassani ‘Mgosi’ wa Simba na Nadir Haroub ‘Cannavaro’ wa Yanga ni miongoni mwa wachezaji 38

wa Simba na Yanga ambao wapo huru kwa kuwa wamemaliza mikataba yao inayotambuliwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Ofisa Habari wa TFF Florian Kaijage jana alitangaza orodha ya wachezaji 155 wa timu mbalimbali ambao ama wametemwa au wamemaliza mikataba yao katika klabu tisa kati ya 12 zitakazoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao.

Katika orodha hiyo ya wachezaji waliomaliza mikataba yapo majina ya Mgosi na Haroub, ambapo awali ilinukuliwa na viongozi wa klabu hizo kongwe nchini kuwa wachezaji hao bado wana mikataba halali na klabu hizo, hivyo hawezi kujiunga na klabu nyingine pasipo kufanya mazungumzo.

Mbali na Mgosi na wachezaji wengine waliomaliza mikataba yao kwa Simba ni Ramadhani Chombo na Jabir Aziz ambao tayari wamejiunga na klabu ya Azam, Mohamedi Banka, Salum Kanoni, Juma Jabu, Kelvin Yondani, Juma Nyoso,Nico Nyagawa, David Naftali na Mohamedi Kijuso.

Wengine ni Haruna Shamte, Adam Kingwande, Ulimboka Mwakingwe, Salim Aziz, George Nyanda, Ally Mustapha, Meshack Abel na Deo Munishi.

Kwa upande wa Yanga wachezaji waliomaliza mikataba yao mbali na Cannavaro ni kipa Obren Cuckovic, Shadrack Nsajigwa, Nurdin Bakari, Abdi Kassim, Godfrey Bonny, Bakari Mbegu, Moses Odhiambo, Kabongo Honore, Boniface Ambani, Hamisi Yusuf, Fred Mbuna,Vicent Barnabas na Ally Msigwa.

Klabu ya Yanga imetangaza kuwatema wachezaji wake Amir Maftah na Mcameroun Robert Mba kwa madai ya utovu wa nidhamu ndani ya klabu hiyo.

Mgosi na Cannavaro wamekuwa wakihusishwa kutaka kujiunga na Azam ya Dar es Salaam.

Katika orodha hiyo wachezaji 23 wa Mibwa wamemaliza mikataba yao, ambapo timu nyingine na idadi ya wachezaji waliomaliza mikataba katika mabano ni Majimaji (25),Toto Afica (9), Kagera Sugar (26), Azam (17), JKT Ruvu (9),African Lyon(8).

Kwa upande wa Azam wachezaji wake waliomaliza mkataba na klabu hiyo imetangaza haitaongeza ni Habibu Mhina, Crispine Odula, Maridadi Haule, Nsa Job, Osborne Monday, Said Sued, Salum Machaku, Yahya Tumbo, Ben Kala na Shaaban Kisiga.

Wachezaji waliomaliza mikataba yao na wapo huru ni Vladmir Niyonkuru, Ibrahim Mwaipopo, Ibrahim Shikanda, Dan Wagaluka, Luickson Kakolaki, Erasto Nyoni na Philip Alando.

Ambani amtabiria makubwa Ngasa


MSHAMBULIAJI wa Yanga, Boniface Ambani amewataka wanachama na mashabiki wa timu hiyo kumpa ushirikiano kiungo mshambuliaji wa Azam FC, Mrisho Ngassa kama alivyokuwa akiitumikia klabu yao.

Ambani ambaye yupo nchini Kenya kwa ajili ya mapumziko ameliambia Championi Ijumaa kuwa, Ngassa asionekane kama msaliti baada ya kutimkia Azam, kwa kuwa viongozi wa timu hiyo walishindwa kumtekelezea mahitaji yake.

kwa mujibu wa gazeti la Champion, “Hakuna mchezaji asiyeipenda klabu yake milele, ni vema mashabiki wakatambua hilo, wanaotakiwa kutupiwa lawama ni viongozi ambao kama wangekuwa na nia ya kumhitaji aendelee kuichezea klabu hiyo naamini wangeweza kumbakisha kwa kiasi chochote.

“Pia itambulike soka ni sehemu ya maisha, kipindi ambacho mchezaji anawika ndiyo hicho cha kukitumia kuliko kuendelea kuchezea timu kwa mapenzi siyo kwa ajili ya maisha ya baadaye,” alisema Ambani ambaye naye amekuwa akihusishwa na mipango ya kuhamia Azam.

Katika msimu wa 2008/2009 Ambani alitwaa tuzo ya ufungaji bora, lakini aliiachia tuzo hiyo msimu uliopita na kwenda kwa Mussa Mgosi.

Papic asema TFF ni wavurugaji


KOCHA wa Yanga, Kostadic Papic amepinga kanuni mpya ya usajili iliyotangazwa na Shirikisho la Soka la Tanzania(TFF) la kusajili wachezaji watano wa kigeni kwa kueleza kuwa kanuni hizo zinavuruga taratibu za klabu.

Kauli ya Mserbia huyo imekuja baada ya TFF kusisitiza kuwa klabu za Ligi Kuu sasa zitaruhusiwa kusajili na kuchezesha wachezaji watano wa kigeni tofauti na msimu uliopita ambapo zilisajili kumi.

Akizungumza na Mwananchi kwa simu kutoka Serbia aliko mapumzikoni, Papic alisema kuwa kitendo cha TFF kutoa sheria ya wachezaji watano wa nje kusajiliwa ni kuzinyima haki klabu ambazo zimekuwa na maandalizi makubwa kwa ajili ya msimu mpya wa ligi na mashindano yanayowakabili.

"Si sahihi kabisa, ligi imeisha tangu mwezi Aprili, kwa nini basi tangu mwezi Machi kabla ya ligi kuisha wangeweka wazi kanuni hiyo ili kila klabu ijue badala ya kusubiri mpaka sasa ndio wanaweka wazi wakati klabu zimeshatumia gharama nyingi kufanya usajili wake,"alisema Papic ambaye anafahamika kama Bill Clinton, raia wa zamani wa Marekani.

Papic ambaye anatarajiwa kurejea nchini Julai 15, siku tatu kabla ya uchaguzi wa Yanga, alisema, "TFF haitendi haki kwa klabu, wachezaji na sisi makocha, hichi kitu wanachokifanya hakuna sehemu yoyote duniani kinafanywa si sahihi na si haki."

Kwa mujibu wa gazeti la Mwananchi, Wiki iliyopita TFF iliweka bayana kuwa utaratibu mpya wa usajili wa kutumia wachezaji watano ni wa kimataifa kwa msimu mpya utakaoanza Agosti 21 badala ya 10 kama ilivyokuwa msimu uliopita.

Kanuni hiyo mpya ya TFF inatoa ahueni kwa wachezaji wa ndani, lakini ni mwiba mchungu kwa klabu za Yanga na Simba ambazo zimesheheni wachezaji wa kigeni.

Mpaka sasa ina wachezaji wanne ambao ni Yaw Berko, John Njoroge, Wisdom Ndlovu na Robert Jama Mba(ambaye ametimuliwa) na kocha wao Papic anatarajiwa kutua nchini na wachezaji wengine watatu ambao ni Kenneth Asamoah, Ernest Boakye, na Isaac Boakye, raia wa Ghana na kufikisha idadi ya wachezaji saba.

Kufuatia kanuni hiyo Yanga italazimika kuwaacha wachezaji wawili wa kigeni ili kwenda sambamba na kanuni hiyo ya TFF.

Kwa upande wa Simba, inao Joseph Owino, Hillary Echesa, Jerry Santo, Mike Barasa, Emmanuel Okwi na Patrick Ochan ambaye ni kiungo, raia wa Uganda na hivyo kulazimika kumwacha mchezaji mmoja kati ya hao.

England out, waishia kulilia goli laLampard

PAMOJA na kupokea kipigo cha kusikitisha cha mabao 4-1 kutoka kwa Ujerumani, England wamemshutumu mwamuzi Jorge Larrionda wa Uruguay aliyekata bao la kusawazisha wakati shuti la kiungo wao Frank Lampard lilipopiga mwamba wa juu na kuanguakia ndani ya mstali.

Bao hilo lilikataliwa na mwamuzi Jorge Larrionda wa Uruguay ikiwa muda mfupi baada ya England kupata bao la kwanza huku Ujerumani ikiongoza kwa mabao mawili, ambapo hata mwamuzi msaidizi Pablo Fandino hakuona mpira kama ulikuwa umevuka mstali wa goli.

Bao hilo lililokataliwa lilipoonyeshwa kwenye marudio ya televisheni ilionekana mpira huo ulivuka mita moja ya mstali wa goli.

Alikuwa ni Frank Lampard ambaye alipiga shuti hilo akiwa mita 40 ambapo kipa wa Ujerumani, Manuel Neur alishindwa kulizuia.

Bao hilo lililokataliwa linafananishwa na bao la tatu la England ambalo lilifungwa na Geoff Hurst mwaka 1966 katika fainali dhidi ya Ujerumani magharibi wakati huo, ambapo wajerumani wanapinga bao hilo halikuvuka mstali na linajadiliwa mpaka leo,katika mechi hiyo England ilishinda 4-2.

Akilizungumzia bao la jana, mwamuzi wa zamani wa Ujerumani Helmut Krug aliiambia televisheni ya Ujerumani kwa England wamekataliwa bao.

"Hilo ni kosa ambalo haliwezi kusameheka, mwamuzi msaidizi alitakiwa kuona, mpira ule ulivuka mstali, mwamuzi msaidizi alitakiwa kuona bila hata ya kurudia kutazama tukio hilo,"alisema Helmut Krug.

Rais wa Shirikisho la soka la Ujerumani Theo Zwanziger aliongeza kwenye mahojiano na televisheni ya Ujerumani wakati wa mapumziko kwamba mwamuzi alitakiwa kuona mpira umevuka mstali pale pale alipokuwepo.

"Tunatakiwa tusimamie sheria za soka tulizonazo, ninaweza kuona kwamba mashabiki wa soka wa England hawakufurahia maamuzi ya mwamuzi kukataa bao, niliweza kuona mpira ule uliingia golini,"alisema Zwanziger.

Tukio hilo litakuwa limechochea uhasama wa timu hizo pinzani England na Ujerumani, pia linatarajiwa litachochea kuanzisha mjadala kwa FIFA kuanza kutumia teknolojia ya video ili kuweza kuwasaidia waamuzi kutatua kutoa maamuzi katika mazingira magumu.

Katika mchezo huo mshambuliaji chipukizi Thomas Mueller alifunga mabao mawili pekee yake baada ya Miroslav Klose na Lukas Podolski kuifungia Ujerumani mabao mawili Ujerumani.

England ilipata bao lake la kufutia machozi lililofungwa na beki Matthew Upson katika dakika 37 England kabla ya bao la Lampard kukataliwa dakika moja baadaye.

JENGO LAU 11
DAKAR; Watu 11 wamepoteza maisha kaskazini mwaSenegal baada ya jengo walilokuwa wamekaa na kuangalia mechi za Kombe la Dunia kuanguka ghafla katika mji wa Matam uliopo kaskazini mwa Darak.

Tukio hilolilitokea wakati mashabik hao wakishudia mechi kati ya Uruguay dhidi ya Korea Kusini.

APS ilimkariri afisa usalama akisema watu wengine wawili wameumia vibaya baada ya kudondokewa na jengo hilo.

Senegal haijafuzu kwa fainali za Kombe la Dunia mwaka huu, lakini mashindano hayo yamekuwa yakiwavuta watu wengi na kufutilia kupitia vituo mbalimbali vya televisheni.

Saturday, June 26, 2010

Wanahabari klabuni Azam FC


Wana habari wakimsikiliza Makamu Mwenyekiti wa Azam FC makao makuu ya Azam FC, hapa ilikuwa siku Azam FC ilipowatambulisha wachezaji wake wapya wa msimu wa 2010/11 makao makuu ya klabu ya Azam FC Mzizima jijini Dar es Salaam

karibu Ngasa

Ngasa kushoto, Mzee Said Mohammed na Jackson Chove, hapa ilikuwa siku ya utambulisho wa wachezaji hawa Azam FC

Azam FC new kit





Azam FC will soon introduce its own jersey and become the first Tanzanian Team to own quality shirts that will also be available for its fans, the jersey will be available in stores across the country,